Breaking News
recent

TUNAKOENDA WAPI, SOMA JINSI RASILIMALI ZA TANZANIA ZINAVYOCHOTWA BUREBURE....




Wawekezaji kutoka nje, wametajwa kugeuka mawakala wa kutorosha fedha nje ya uchumi wa Tanzania, kiasi cha mabilioni ya Dola za Marekani, ambayo yakibadilishwa, yanafikia matrilioni ya Shilingi.
Fedha hizo zimekuwa zikiporwa nchini kutoka serikalini kwa maana ya kukwepa kodi na katika jamii, kupitia ununuzi wa bidhaa nje ya nchi, ambazo thamani yake huchakachuliwa kwa kuongezwa kinyume na thamani halisi.
Hayo yamo katika Ripoti ya Shirika la Global Financial Integrity (GFI), iliyotolewa jana (May 19,2014) mbele ya Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato (TRA), Rished Bade na Gavana wa Benki Kuu (BoT), Profesa Benno Ndulu.
“Biashara hii inayofanyika kwa kificho kwa kutumia mifumo ya kihasibu, imekuwa ikipora serikali na jamii fedha zinazohitajika kwa ajili ya kukuza sekta binafsi, ujenzi wa miundombinu na kutoa huduma muhimu.
Tafsiri yake, biashara hii imekuwa ikiondoa fursa za maendeleo, nafasi za ajira na lulu ambazo zinapotea kiuchumi,” imeeleza ripoti hiyo.
“Zaidi ya Dola za Marekani bilioni 8 (zaidi ya Sh trilioni 10) katika mzunguko wa fedha zimehamishwa nje ya uchumi wa Tanzania isivyo halali kati ya 2002 na 2011,” imeeleza ripoti hiyo.
Pia, imefafanua kuwa Serikali ya Tanzania katika muda huo, imekuwa ikipoteza mapato ya kodi ya wastani wa dola za Marekani milioni 248 kila mwaka katika biashara, ambayo kodi hazikulipwa.
Katika mahesabu jumuishi ya mtaji ghafi uliohamishwa katika uchumi wa Tanzania isivyo halali (cumulative growth illicit flows), kupitia biashara hii ni dola za Marekani bilioni 18.73 kutoka 2001 na 2011, na sehemu kubwa ilihamishwa katika miaka mitano ya mwisho ya muda huo,” imeeleza taarifa hiyo.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, katika ununuzi kutoka nje, wawekezaji hao wamekuwa wakishirikiana na wauzaji, kudanganya thamani ya bidhaa walizonunua kutoka nje kuwa ni ya juu, kuliko thamani halisi.
Matokeo yake, wawekezaji hutumia mwanya huo kuhamisha fedha nyingi za kigeni kwenda nje ya nchi, kwa jina la kununua bidhaa za thamani kubwa, kumbe wamenunua bidhaa za thamani ndogo na fedha nyingine inakuwa imetoroshwa nje ya nchi isivyo halali.
“Makadirio ya fedha zilizohamishwa katika uchumi wa Tanzania kwa kupitia mfumo huu wa kudanganya thamani ya ununuzi wa bidhaa kutoka nje, yanaonesha sehemu kubwa ya fedha hizo zimehamishwa katika ununuzi wa mafuta ambayo yamesamehewa kodi katika kampuni za madini.
Ufafanuzi wa hili ni kwamba, inaonekana kampuni za madini, zimekuwa zikichakachua kwa kuongeza thamani ya gharama zao za ununuzi wa bidhaa na huduma kutoka nje, ili kuhamisha mtaji isivyo halali,” imeeleza taarifa hiyo.
Sehemu nyingine ambayo imetajwa kuwa uchochoro wa kutorosha fedha nje ya nchi, ni miradi iliyo katika Ukanda Maalumu wa Uwekezaji (EPZ), ambayo imepewa msamaha wa kodi (import duty) katika malighafi zitakazoagizwa kwa ajili ya kuzalisha bidhaa za hapa nchini, pamoja na msamaha wa kutolipa kodi (corporate tax) kwa miaka 10.
BOT, TRA na PAC wanena Gavana wa Benki Kuu (BoT) , Profesa Benno Ndulu alisema ripoti hiyo ni muhimu, kwa vile imewazindua macho juu ya udanganyifu, unaofanywa na wafanyabiashara wa kutorosha fedha na kuingiza nchini fedha haramu.
"Tuchotakiwa ni kufanya kazi kubaini namna kampuni hizi za kutoka nje zinavyotoa taarifa za uongo ili watoroshe fedha hasa katika eneo la mafuta," alisema Ndulu.
Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato (TRA), Rished Bade alisema ripoti ya GFI itaifanya mamlaka yake, kutafuta mbinu za kupambana na tatizo hilo la biashara zisizo na ankara halali, kushamiri na kuifanya nchi kupoteza mabilioni ya fedha.
Alisema TRA imeshangazwa na wawekezaji kutoka nje, kukwepa kodi kwa kutoa takwimu za uwongo juu ya bidhaa wanazonunua huko ambazo wanasamehewa kodi na namna wanavyotumia takwimu hizo za uwongo kuingiza fedha haramu nchini.
Alisema TRA kwa sasa inahangaika ili kuingia kwenye mkataba mkubwa wa kimataifa, ambao utaisaidia mamlaka hiyo kubaini udanganyifu huo kwani utawezesha mamlaka kuwasiliana na bidhaa zinakoenda kuuzwa na zinakotoka kuingia nchini.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), Kabwe Zitto alisema kuingizwa na kutolewa nchini kwa fedha haramu kunatokana na misamaha ya kodi ambayo inatolewa kiholela na Serikali.
"Ripoti imedhihirisha kuwa misamaha ya kodi kwa wawekezaji hawa kumetoa mianya ya wawekezaji hawa kutoa takwimu za uwongo kuonesha kuwa wamenunua bidhaa hizo kwa bei kubwa wakati ni uwongo," alisema Zitto.
 
Chanzo:- Habari Leo
Unknown

Unknown

No comments:

Powered by Blogger.