Breaking News
recent

MENEJA WA EWURA, KIFO CHAKE UTATA MTUPU, MWILI WAKE WAAGWA LEO KABLA YA KUPELEKWA KIJIJINI KWAO...


Aaliyekuwa Meneja Biashara ya Mafuta wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (Ewura), Julius Gashaza aliyefariki dunia May 18,2014, anatarajiwa kuagwa leo(May 20, 2014) nyumbani kwake Yombo Vituka, Dar es Salaam kabla ya kusafirishwa kwenda nyumbani kwao  Murukulazo,wilayani Ngara,mkoani Kagera kwa Mazishi Al hamisi May 22, 2014.
Awali ndugu huyo ambaye alikataa kutajwa gazetini, alisema kuwa kifo cha Gashaza ni pigo kubwa kwa familia hiyo, lakini hawana cha kufanya zaidi ya kuachia Polisi kufanya kazi yao.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi Mkuu wa Ewura, Felix Ngamlagosi, Gashaza aliajiriwa na mamlaka hiyo 2006 akiwa Mkaguzi Mkuu wa Mafuta ya Petroli. Mwaka 2013 Gashaza aliteuliwa kuitumikia Mamlaka hiyo katika cheo cha Meneja wa Biashara kwenye Idara hiyo ya Petroli.
Taarifa hiyo ilieleza kuwa mnamo Mei 15, mwaka huu Gashaza alisafiri kwenda Dodoma kwa usafiri wa ndege akimwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa Ewura kwenye kikao cha Kamati ya Bunge ya Bajeti.
"Baada ya kikao hicho, alirejea jijini Dar es Salaam Jumamosi Mei 17, 2014 saa tatu usiku. Asubuhi ya siku iliyofuata, tarehe 18 Mei 2014, uongozi wa Ewura ulipokea taarifa za kushtua toka kwa familia yake kwamba Gashaza amefariki dunia," ilieleza taarifa hiyo.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Temeke, Engelbert Kiondo akizungumza  wa mkutano na waandishi  Dar es Salaam jana. Picha na Salhim shao. 
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Temeke, Engelbert Kiondo, alisema Gashaza alikutwa amejinyonga kwenye nyumba ya kulala wageni ya Mwangaza Lodge kwa kutumia tai aliyoiunganisha na waya wa pazia na kuitundika kwenye nondo za dirisha la chumba namba 113.
Kamanda Kiondo alisema chanzo cha kifo chake hakijafahamika lakini inasadikiwa kuwa siku ya Mei 17, aliwaeleza ndugu zake kuwa ana matatizo ya kiofisi ambayo hata hivyo hakuyaweka wazi.
Sintofahamu imeendelea kugubika kifo cha Gashaza na sasa imeelezwa kuwa alirudi kutoka Dodoma akiwa amejawa hofu na kukosa amani.
Aidha kukiwa na utata wa kifo cha Meneja wa Biashara ya Petroli wa Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (Ewura), imebainika kuwa tofauti ya takwimu kati ya mamlaka hiyo na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), iliyotolewa kwenye Kamati ya Bunge ya Bajeti ni Sh25 bilioni.
Meneja huyo, Julius Gashaza alikuwa akihudhuria kikao kilichokuwa kikijadili tofauti hiyo bungeni Dodoma na baadaye aliporudi Dar es Salaam akakutwa amejinyonga hotelini huku ikielezwa kuwa alirudi akiwa amejawa hofu na kukosa amani.
Vyanzo vyetu ndani ya kamati hiyo vimeeleza kuwa tofauti iliyobainika katika hesabu za taasisi hizo za Serikali ni lita 11,755,161, ambazo zingeuzwa kwa bei ya sasa ya petroli mkoani Dar es Salaam ya Sh2,200 zingepatikana Sh25.86 bilioni.
Kwa mujibu wa vyanzo hivyo, takwimu za TRA zinaonyesha kuwa kati ya Julai 2013 hadi Machi mwaka huu, kiasi cha mafuta kilichoingizwa nchini kilikuwa lita 2,189,240,000 wakati Ewura ilionyesha ni lita 2,177,484,839.
Hata hivyo, baada ya utata huo na Kamati ya Bajeti chini ya Andrew Chenge kuitaka Serikali itoe ufafanuzi wa tofauti hizo, Serikali iliwasilisha taarifa yake Jumapili ikisema takwimu zote ni sawa.
Katika ufafanuzi wake, Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba alisema uhakiki wa takwimu hizo ulibaini kuwa zote zilikuwa ‘sahihi’ na kwamba tofauti iliyopo inatokana na upimaji wa mafuta.
Nchemba alikaririwa akisema TRA hupima mafuta kwenye meli mara inapoingia na kukadiria kodi wakati Ewura hupima mafuta yanapopokewa kwenye matanki.
“Kwa kuwa wakati mwingine meli hutumia muda mrefu tangu zinapoingia hadi zinapoteremsha mafuta, sehemu ya mafuta ambayo TRA huhesabu kama yameingizwa katika mwezi mmoja wakati Ewura hupata takwimu za kiasi cha baadhi ya mafuta hayo katika mwezi unaofuata na hiyo ndiyo iliyosababisha kuwapo kwa tofauti hiyo ambayo hata hivyo ni ndogo.”
Kulingana na takwimu hizo, kiasi cha mafuta kilichoonyeshwa na TRA kilikuwa juu kuliko kile kilichoonyeshwa na Ewura na haijajulikana iwapo kutofautiana huko kwa takwimu kuliifanya Serikali kumweka kitimoto Gashaza.

Uchunguzi wa Jeshi la Polisi.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Temeke, Engbert Kiondo alisema uchunguzi wa chanzo cha kifo hicho unaendelea kwa kuangalia maeneo matatu.
Alisema utajielekeza kubaini kama kulikuwa na mgogoro wowote wa kifamilia au iwapo alikuwa na tatizo lolote kazini kwake kabla ya kifo chake na mazingira kilipotokea kifo hicho na baada ya kujiridhisha watatoa taarifa kamili kwa vyombo vya habari.
Kuna maswali mengi ya kujiuliza kwa nini hakutaka kulala nyumbani kwake usiku ule badala yake akaamua kulala hotelini, tunafanya upelelezi kubaini nini hasa kilimsukuma kujinyonga,” alisema.
Alisema pia wanasubiri ripoti ya uchunguzi ya daktari ambayo wataitumia katika upelelezi wao kubaini chanzo.
Alisema polisi watachunguza kama Gashaza alijinyonga kweli au aliuawa na kutengenezewa mazingira ya kujinyonga.
Utata Bungeni.
Wakati inaelezwa kuwa kulikuwa na tofauti ya takwimu kati ya zile za TRA na Ewura kuhusu kiwango cha mafuta kilichoingia kwenye soko, taarifa zaidi zimeeleza kuwa katika kikao cha Kamati ya Bajeti, Gashaza hakuulizwa swali hata moja.
Mmoja wa wajumbe wa kamati hiyo alisema marehemu hakuhojiwa labda kilichomfanya ajiue ni hofu iliyotokana na mahojiano baina ya kamati hiyo na watendaji wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA).
Alisema kamati hiyo iliwaita viongozi wa Wizara ya Fedha na Wizara ya Nishati na Madini ili kuwahoji kwa nini Sh50 zilizoongezwa katika mafuta ya petroli na dizeli hazikwenda REA?
Mjumbe huyo alisema kati ya zaidi ya Sh100 bilioni zilizotakiwa kwenda Rea ni Sh17 bilioni tu zilizopelekwa na fedha nyingine zilielekezwa kwenye matumizi mengine ambayo hayakuidhinishwa na Bunge.
Unknown

Unknown

No comments:

Powered by Blogger.