Breaking News
recent

ISRAEL YAAPA KULIPIZA KISASI KWA HAMAS



Benyamin Netanyahu,waziri mkuu wa Israel
Israel imeapa kulipiza kisasi dhidi ya kikundi cha wapiganaji wa Hamas wa Kipalestina wanaosemekana kuwateka na kuwaua vijana watatu katika eneo la Ukingo wa Magharibi wa mto Jordan.
Miili ya vijana hao Naftali Frenkel, Gilad Shaar na Eyal Yifrach ilionekana Jumatatu jioni, baada ya kupotea kwa zaidi ya wiki mbili.
Waziri Mkuu wa Israel, Benyamin Netanyahu amesema: "Hamas wanahusika na Hamas watalipa." Hamas wanakanusha kuhusika na tukio hilo.
Israel imefanya mashambulio ya anga zaidi ya 30 katika Ukanda wa Gaza usiku kucha.
Miili ya vijana watatu waliotekwa na kuuawa ilipatikana karibu na mji wa Halhul
Mashambulio hayo yamekuja ikiwa ni kujibu mashambulio 18 ya maroketi kutoka Gaza tangu Jumapili usiku, limesema jeshi la Israel.
Majeshi ya Israel pia yamesambaa katika mji wa Palestina wa Halhul. Miili ilipatikana chini ya kifusi cha miamba karibu na mji huo. Afisa mmoja wa Israel anasema inaonekana kuwa vijana hao watatu waliuawa kwa kupigwa risasi mara baada ya kutekwa kwao.
Israel imewataja watuhumiwa wawili wa utekaji wa vijana hao kuwa ni Ayoub al-Kawasma na Abu Aisheh. Jeshi la Israel limesema lilitegua milipuko iliyokuwa imetegwa wakati wa kuzivamia nyumba za watuhumiwa hao.
Askari wa Israel walitegua milipuko katika nyumba za watuhumiwa wawili wa Hamas. Picha zimeonyesha uharibifu mkubwa uliofanyika katika nyumba ya Abu Aisheh.
Mpalestina mmoja pia aliuawa baada ya kuwarushia kilipuzi wanajeshi wa Israel waliokuwa katika operesheni katika mji wa Jenin ulioko magharibi mwa mto Jordan, mapema Jumanne, limesema jeshi la Israel.
Unknown

Unknown

No comments:

Powered by Blogger.